Kwa mujibu wa taarifa, wananchi wa Bahrain waliandamana Jumapili katika maeneo mbali mbali nchini huo huku wakitoa nara za kupinga na kulaani mapatano baina ya serikali ya nchi hiyo na utawala wa Kizayuni wa Israel.
Harakati ya Kiislamu ya Al-Wifaq ya nchini Bahrain imesema makubaliano yoyote yale yaliyosainiwa bila ya kuidhinishwa kwa kura za wananchi ni batili na hayana uhalali wa kisheria na ikaongeza kuwa, zaidi ya asilimia 95 ya wananchi wa Bahrain wanapinga kuanzishwa uhusiano wa kawaida kati ya Manama na Tel Aviv.
Jana ujumbe wa pamoja wa Israel na Marekani ulifika mjini Manama kukamilisha rasmi makubaliano ya kupanua ushirikiano kati ya utawala wa Bahrain na utawala wa Kizayuni.
Tarehe 15 Septemba mwaka huu, Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Bahrain walitia saini makubaliano ya kutangaza uhusiano wa kawaida baina ya nchi zao na utawala ghasibu wa Israel.
Sherehe hizo zilizofanyika katika Ikulu ya Marekani, White House, zilihudhuriwa pia na rais wa Marekani, Donald Trump na Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala dhalimu wa Israel.
Tangu Februari mwaka 2011, wakati ulipoanza mwamko wa Kiisamu Asia Magharibi, Bahrain imekuwa uwanja wa maandamano ya amani ya wananchi wanaopinga utawala wa kifalme wa ukoo wa Aal Khalifa. Wananchi hao wanataka kuwepo uhuru, utekelezwe uadilifu, ukomeshwe ubaguzi na kuundwa serikali itakayochaguliwa na wananchi wenyewe.