Sayyid Hassan Nasrullah alitoa mwito huo jana Jumanne na kusisitiza kuwa, serikali mpya ya Beirut inapaswa kuwaondolea wananchi wa Lebanon dhiki ya nishati ya umeme.
Amesisitiza kuwa, "nchi kadhaa za Mashariki na Magharibi zimetangaza azma zao za kupatia ufumbuzi matatizo ya umeme nchini Lebanon, kadhia hiyo inapaswa kutatuliwa. Iran ndiyo nchi pekee ambayo ipo tayari kuunda vituo vya nishati nchini Lebanon."
Sayyid Nasrullah ameliasa Baraza la Mawaziri la nchi hiyo lichangamkie ofa iliyotolewa hivi karibuni na Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ya kupatia ufumbuzi mgogoro wa nishati ya umeme unaoisumbua Lebanon kwa sasa.
Hadi sasa Iran imetuma meli tatu za mafuta nchini Lebanon kupitia Syria ili kuisaidia nchi hiyo ambayo ilikuwa inakumbwa na uhaba mkubwa wa bidhaa hiyo.
Viongozi mbalimbali wa Lebanon wakiwemo wa kisiasa na kidini wamekuwa wakisisitiza kuwa, kutumwa meli za mafuta za Iran nchini humo kumewezesha kuvunjwa mzingiro wa Marekani dhidi ya nchi hiyo.