IQNA

Ibada ya Hija

Waislamu Uingereza wachanganyikiwa na sheria mpya za Saudia kwa wanaotaka kuhiji

15:34 - June 27, 2022
Habari ID: 3475434
TEHRAN (IQNA) - Waislamu wa Uingereza yamkini hawataweza kutekeleza ibada ya Hija mwaka huu baada ya kusibiri kwa muda wa miaka wakati Hija ilikuwa marufuku kwa walio nje ya Saudia kutokana na janga la corona.

Saudi Arabia ilitangaza hivi karibuni kuwa,  mahujaji kutoka nchi Magharibi wanaokusudia kushiriki katika Ibada ya Hija mwaka huu lazima sasa watume maombi kupitia tovuti ya serikali.

Uamuzi huo utaondoa jukumu la mashirika ya usafiri katika mchakato huo. Baada ya miezi kadhaa ya sintofahamu miongoni mwa wanaotarajia kuwa Mahujaji katika nchi za Magharibi kutokana na ukimya wa mamlaka ya Saudia kuhusu maeneo waliyotengewa wakati wa Hija, Wizara ya Hija ya Ufalme ilithibitisha wiki hii kwamba Waislamu katika nchi  "Ulaya, Marekani na Australia" lazima wawasilishe maombi yao kupitia tovuti ya kiserikali ya Motawif.

Mwanamke mmoja alielezea mchakato huo ambao unawalenga Waislamu walio katika nchi za Magharibi kuwa "mateso" baada ya ndoto zake za kukamilisha moja ya nguzo za Uislamu kupokonywa kutokana na mahitaji mapya yaliyowekwa na utawala wa Saudia.

Hija ni wajibu kwa kila Mwislamu mwenye uwezo lakini kutokana na gharama zinazozidi kuongezeka inamaanisha kuwa watu wengi mwaka huu hawawezi kuhiji hata baada ya kuweka akiba kwa miaka mingi.

Matumaini ya wengi Kuhiji mwaka huu yamefifia baada ya Saudi Arabia kuanzisha sheria hiyo mpya inayowalazimi wasafiri watarajiwa kutenga  nafasi kupitia tovuti ya serikali, mchakato ulioelezwa na wengine kuwa ni sawa na bahati nasibu.

Waislamu milioni moja wataruhusiwa kukamilisha Hajj, ambayo itafanyika Julai, na wote lazima wapate chanjo mara tatu na wawe na umri wa chini ya miaka 65. Hiyo ni chini ya nusu ya watu milioni 2.5 waliohudhuria mwaka wa 2019.

Suhail Sherwani, daktari  kutoka kusini mwa London, alisema yeye na familia yake walilipia safari ya Hajj katika majira ya kuchipua mwaka huu kupitia wakala wa usafiri. Hata hivyo, baada ya Saudia kutangaza kuwa mabadiliko yatafanyika, nafasi aliyokuwa amejitengea yeye na familia yake ilibatilishwa na akarejeshewa fedha alizokuwa amelipa

Mawakala wa usafiri wa Hija kwa kawaida hupanga safari za ndege, malazi na visa pamoja na kuandaa miongozo na mikusanyiko ili kuwasaidia mahujaji kujiandaa kwa ajili ya shughuli hii muhimu ya kiroho.

Hata hivyo, mawakala hawa wa usafiri sasa wametupiliwa mbali kama baada ya Saudi kutangaza kwamba kuhifadhi kunaweza tu kufanywa kupitia tovuti yao wenyewe iitwayo Motawif, iliyopewa jina la mfumo wa "bahati nasibu" ya Hajj mtandaoni.

Baada ya kujiandikisha kwenye tovuti , waliambiwa wangefahamishwa ndani ya wiki moja kuhusu hali ya ombi lao. Iwapo wangefaulu, wangeweza kuchagua kifurushi na kufanya malipo, baada ya hapo Motawif ingewatumia e-visa.

Dkt Sherwani alituma maombi kupitia tovuti ya Motawif na akapokea ujumbe kwamba ombi lake lilifaulu, na kuulizwa kufanya malipo yote.

Lakini baada ya kulipa, alipokea ujumbe ukisema kuwa ombi lake halijafauli licha ya pesa kutoka kwenye akaunti yake.

Sasa yuko gizani, hana uhakika ikiwa ameangukia kwenye maswala ya kiufundi, ikiwa atarejeshewa pesa na ikiwa atapata fursa nyingine ya kuingia kwenye bahati nasibu.

Lakini mawakala wa usafiri ana matumaini kwamba waendeshaji watalii wa Uingereza watarejeshwa mwaka ujao kwa sababu ya kiwango cha kuchanganyikiwa wateja

Huku mahujaji wa kwanza kutoka sehemu mbalimbali za dunia wakiwa tayari wamewasili Makka na siku chache zimesalia kabla ya ibada kuanza, wengi wamekubali shingo upande kwamba hawatafika Makka mwaka huu na sababu kuu ni sheria hizo mpya zilizowekwa na wakuu wa Saudia.

3479478

captcha