Katika taarifa iliyotolewa Ijumaa, ofisi ya vyombo vya habari ilisema vita vya mauaji ya kimbari vya Israel dhidi ya Gaza, vilivyoanza mwezi Oktoba, hadi sasa vimeua wanawake 8,900 wa Kipalestina na kujeruhi wengine zaidi ya 23,000, huku 2,100 wakiwa bado hawajulikani walipo.
“Tarehe 8 Machi, dunia inaadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanawake, kuwaenzi wanawake kwa mafanikio na mapambano yao. Hata hivyo, wanawake wa Kipalestina wanaendelea kulipa gharama kubwa kwa ajili ya uhuru na utu.”
Taarifa hiyo ilisema Israel inawaua wanawake wa Kipalestina wakati "ulimwengu umesimama kando, ukishuhudia ukiukwaji huu mkubwa dhidi ya wanawake wa Palestina bila kuinua kidole."
Ofisi hiyo ilibainisha kuwa vita vya Israel pia vimewalazimisha zaidi ya wanawake nusu milioni wa Kipalestina kuyahama makazi yao na kuishi chini ya "matatizo makubwa", bila kupata mahitaji ya kimsingi kama vile chakula na dawa.
Kulingana na taarifa hiyo, vita hivyo pia "vimefanya wanawake 60,000 wajawazito kuishi maisha magumu mno, wakikosa mahitaji ya kimsingi ya afya na matibabu". Ofisi hiyo ilisema mamia yao “wamepoteza wana wao, watoto wachanga, au watoto ambao hawajazaliwa kwa sababu ya kulipuliwa kwa mabomu, woga, na mauaji yanayotekelezwa na ‘Waisraeli’.”
Taarifa hiyo pia ilirejelea masaibu ya wafungwa wa kike wa Kipalestina, ikisema makumi kadhaa "wanakabiliwa na mateso ya kimwili na kisaikolojia, kutendewa vibaya na kudhalilishwa."
Ofisi ya vyombo vya habari ilipongeza "uthabiti" wa wanawake wa Kipalestina, ikisisitiza kwamba "wanahitaji sana kutetea haki zao na mahitaji ya maisha badala ya kuuawa, kupigwa risasi, kuwekwa kizuizini, na kulazimishwa kuhama.”
Tangu kuanza kwa mashambulizi ya utawala haramu wa Israel dhidi ya Gaza, jeshi la utawala huo limeua zaidi ya Wapalestina 30,000 na kuwajeruhi wengine zaidi ya 72,000.
Maelfu zaidi pia hawajulikani walipo na inakisiwa kuwa wamekufa chini ya vifusi huko Gaza.
3487472