IQNA

Kiongozi wa HAMAS afika Lebanon baada ya miaka 27

13:13 - September 02, 2020
Habari ID: 3473130
TEHRAN (IQNA) – Kiongozi wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (HAMAS) Ismail Haniya, amefika nchini Lebanon kwa mara ya kwanza baada ya miaka 27.

Haniyah aliwasili Lebanon Jumanne kwa ajili ya mazungumzo na maafisa wan chi hiyo kuhusu mapatano yaliyotiwa saini hivi karibuni baina ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na utawala wa Kizayuni wa Israel kuhusu kuanzishwa uhusiano wa kawaida baina yao.

Hii ni mara ya kwanza kwa Haniya kufika Lebanon tokea mwaka 1993 wakati alipoondoka katika kambi ya wakimbizi alimokuwa akiishi nchini humo.

Haniya anatazamiwa pia kuzitembelea nchi kadhaa za Ghuba ya Uajemi kujadili kadhia hiyo ya kuanzishwa uhusiano baina ya utawala haramu wa Israel na UAE.

Rais wa Marekani, Donald Trump amekuwa akifanya njama za kila namna za kuhakikisha nchi za Kiarabu zinakuwa na uhusiano wa kawaida na utawala pandikizi wa Israel. Siku ya Alkhamisi ya tarehe 13 Agosti, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na utawala wa Kizayuni zilifikia makubaliano ya kuanzisha uhusiano kamili wa kidiplomasia baina yao.

Si hayo tu, lakini vile vile viongozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu wameanzisha pia safari za moja kwa moja za ndege baina yake na utawala wa Kizayuni na ndege ya kwanza ya shirika la El Al la utawala bandia wa  Israel ilitua jana Jumatatu katika uwanja wa ndege wa Abu Dhabi nchini UAE.

3920386

captcha