Idara ya Wakfu ya Serikali ya Ansarullah yenye makao yake Sanaa, Yemen imelaani vikali kitendo cha magaidi hao kubomoa baadhi ya maeneo ya jengo la Msikiti wa Al Nour katika eneo la Al Qataba katika wilaya ya Al Kokha mkoani Al Hudaydah.
Idara ya Wakfu ya Yemen imetangaza kundi la kigaidi la Al-Qaeda lenye mfungamano na Saudi Arabia limeharibu sehemu kubwa ya msikiti huo wa kihistoria.
Taarifa iliyotolewa na Idara ya Wakfu ya Yemen imesema kuwa: Kitendo hicho kiovu kimeongeza jinai nyingine katika faili jeusi la muungano wa wavamizi na mamluki wa katika kadhia ya uharibifu wa mamia ya misikiti ya kihistoria na maziara ya kidini nchini Yemen.
Taarifa hiyo inasema: Kitendo cha washirika wa Saudi Arabia cha kubomoa msikiti wa kale wa al Nour wenye umri wa miaka 700 kimefanyika kwa shabaha ya kuharibu utambulisho wa kidini, kihistoria na kiutamaduni na turathi ambazo ni ushahidi wa ustaarabu wa taifa la Yemen katika kipindi chote cha historia.
Idara ya Wakfu ya Yemen imeziomba jumuiya za kimataifa zinazolinda turathi za binadamu na kiutamaduni kulinda athari na maeneo ya kihistoria na ya kale, na miji ya kihistoria ya nchi hiyo dhidi ya mashambulizi ya kikatili ya wavamizi na mamluki wa Saudi Arabia.
Utawala wa kifalme wa Saudi Arabia uliivamia ardhi ya Yemen mwaka 2015 ikisaidiwa na Marekani na washirika wake wa Kimagharibi na Kiarabu, na hadi sasa maelfu ya raia wasio na hatia wa Yemen wameuawa na mamilioni ya wengine wamelazimika kuwa wakimbizi ndani na nje ya nchi hiyo.
3479645